Wednesday, December 22, 2010

Nyumba Bora kwa Kila Familia Tanzania

NINAAMINI kwamba kila familia ya Kitanzania inastahili, ina haki na inaweza ikawa na nyumba bora ya angalau vyumba viwili kwa kuanzia.

Lakini siamini hili linaweza kufanyika kwa kushusha bei ya vifaa vya ujenzi peke yake bali pia kwa mikakati maalum yenye msukumo toka serikalini, mabenki na wahisani wengine wanaotaka kuufuta kabisa umaskini wa kupindukia hapa nchini.

Ndoto hii inaweza ikatimia sio kwa kuwapa watu nyumba bure bali kwa wao wenyewe kutoa mchango wa aina moja au nyingine katika kufanikisha hili. Aidha, kama tunavyofahamu sekta ya ujenzi hutoa ajira nyingi kwa vijana. Dhamira ya kuipatia kila familia nyumba bora hapa nchini itakwanda mbali sana katika kuwapa ajira vijana kwenye mikoa mbalimbali na wakati huo huo kuwawezesha na wao pia kuwa ni wamiliki wa nyumba.

Stori za saiti na watu kujenga nyumba kila uendako zitakuwa ni stori zilizopitwa na wakati kwani sasa watu watakuwa wanashughulika na yale yanayoongezea utajiri nchi na sio tu ujenzi wa nyumba.

Kwa maneno mengine, jambo linaloonekana kuwa leo ni tatizo, yaani, wananchi kukosa nyumba bora, kwa kutumia ushauri huu, fumba na kufumbua litageuka kuwa ni fursa ya ajira kwa mamilioni ya vijana nchini; ujenzi wa nyumba bora na ubadilishaji wa makazi na mandhari ya nchi toka ile ya shida na umasikini kwenda kwenye ile inayoonesha kwamba angalau watu wetu wanasetirika na wanaishi kwenye nyumba ambazo hawatasita kumkaribisha mgeni.

Katika matangazo yanayonikera sana hapa nchini ni pamoja na lile ambalo linaonekana kushangiliaumasikini wa wananchi vijijini kwa kuonesha nyumba ya udongo iliyoezekwa kwa majani.
Na eti wanaoishi humo wana afya na wanawiri kwa sababu wanatumia chandarua kilichotiwa dawa !
Tangazo hilo linahusiana na matumzi ya neti kupinga malaria. Halinikeri kwa kuwa lina uongo zaidi ya ukweli kwa kuwa malaria haiwezi kutoweka kwa kutumia neti tu, lakini zaidi ni ile hali ya kuonesha kuwa vyandarua vilivyotiwa dawa ni bora kuliko nyumba kwa wananchi vijijini. Hili limenishinda kumeza. Na ninalitema kama lilivyo.

Kama kuna zawadi ya mwaka mpya ambayo ningelipenda Watanzania wenzangu wanaoishi katika manyatta, tembe, msonge na kadhalika wapate ni ile ya uhakika kuwa nchi sasa imedhamiria kila familia iwe na nyumba bora kwa kutumia vifaa, nguvu-kazi, na rasilimali zetu wenyewe papa hapa nchini

Usanii au utangazaji unaosherehekea na kutukuza alama za umasikini wetu, ninaamini, zinaweza kuwa ni kikwazo katika kumwelewesha mwananchi kuwa hali aliyo nayo sasa haikubaliki na hakuhumiwa wala kuumbwa katika dhiki na uhitaji.

Baada ya kubaini kuwa Tanzania haina fedha, Baba wa Taifa, Mwalimu J. K. Nyerere hata hivyo aligundua kuwa akili na nguvu za Watanzania zikielekezwa katika kuboresha maisha yao kwa njia mbalimbali ni sawa na fedha au mtaji wenye thamani wakati mwingine sawa na ule wa pauni au dola za nje.

Kwa maneno mengine, Nyerere kama mwanasaikolojia alijua kuna matumaini au matarajio katika mioyo ya watu wake; kisha kwa kutumia kipaji cha kuzungumza na watu wa hali zote akaweza kuwaunganisha Watanzania kiasi cha kuwa na ndoto moja ya maendeleo na ustawi; na kisha kwa kutambua hatuna fedha, akaamua akili na nguvu za wananchi wake ndizo mtaji muhimu kuliko wote endapo nchi hii kweli inataka iondokane na umaskini. Ili mradi akili na nguvu hizo hazitumiki kuwanufaisha na kuwatajirisha watu wachache tu miongoni mwetu.

Kwa bahati baada ya kuondoka yeye utawalani viongozi waliofuatia aidha wamesahau kabisa juu ya rasilimali hii au wameufanyia usanii kama vile kuita 'mtaji wa masikini ni nguvu zake mwenyewe' lakini mtaji huu haujaelekezwa katika kuleta mabadiliko ya kimaisha tunayoyataka yawepo hapa nchini.

Fursa kwa wananchi kutumia nguvu na akili zao kupunguza umaskini kwa kiasi kikubwa bado zipo. Tofauti tu na miradi ya kupunguza umaskini iliyopo hivi sasa jambo linalotakiwa ni kuwa na miradi ambayo fedha zote zinakwenda kwa maskini wenyewe moja kwa moja kwa njia ya mishahara na malipo ya bidhaa au kazi mbalimbali watakazozifanya. Kwa maneno mengine, fedha na misaada ya kuwaondoa masikini kutoka kwenye umasikini zisitumike kuwatajirisha wanasiasa, maofisa wa serikali na maofisa wa mashirika yasiyo ya kiserikali.

Ujamaa na Kujitegemea unaweza usihitajike katika maeneo mengine, lakini katika hili la lujenzi wa nyumba na makazi bora ya watu bado sera hiyo ni muhimu kama ikitazamwa na kupangwa upya kwa manufaa ya wananchi wenyewe na sio walanguzi wa kisiasa na kiserikali.

Hata hivyo, ni dhahiri kuwa kwa wasiojua na wasioelewa kinachoendelea katika nchi yetu sio rahisi mpango au programu ya kuondoa kiukweli umaskini kukubalika hapa nchini.

Binafsi ninaamini kwamba kuwezesha kila familia nchini kuwa na nyumba bora ya hata vyumba viwili ndio njia bora zaidi ya kupambana na umaskini kuliko yoyote iliyopo hivi leo.

Ila njia hii ni lazima itapigwa vita kwa sababu kadhaa. Kwanza, inamkomboa mwananchi nawanasiasa wadanganyifu wanaoendelea kuwa madarakani kutokana nawananchi kuwawajinga, wasio na afya bora na masikini wa kutupwa; inawapa wananchi uwezo na uhuru zaidi kijamii, kisiasa na kiuchumi; kitendo cha kushiriki katika ujenzi wa nyumba ya kwanza humpanua sana mtu akili na matazamio yake na inaleta ajira kwa jumuiya na kupunguza umaskini.

Ni njia ambayo pia huwawezesha wananchi wa kawaida kufunguka macho na wakatambua kwamba wanastahili kuwa wamilikaji wa nyumba na sio wapangaji tu; wanastahili kuwa nacho kama walio nacho walivyo na ndio njia sahihi zaidi ya kumtoa Mtanzania kwenye umaskini wa kutupwa na unaonuka hadi nje ya mipaka yetu.

Nyumba na Mkakati Dhidi ya Umasikini

Nchi yetu ina mikoa 30 hivi sasa. Pendekezo langu ni kuigawa mikoa hiyo katika mafungu matatu, yaani, kila kundi likiwa na mikoa 10.

Nyumba ina sehemu kubwa tatu. Sehemu hizo ni msingi na kuta; halalfu paa na dari na tatu, milango, madirisha na samani mbalimbali.

Kinachohitajika kufanyika ni kwa vijana wa mikoa kumi ya kwanza kushughulika na uzalishaji matofali, hususan yale ya kuchoma na yale ya mchanga. Au matofali ya kukatwa toka kwenye majabali laini. Matofali hayo yatanunuliwa na serikali kwa ajili ya usambazaji nchi nzima. Matofali hayo yatasambazwa kote nchini kwa ujenzi katika programu yetu ya Nyumba kwa kila familia.

Ndivyo itakavyokuwa pia kwa utengenezaji wa vigae au mabati au kifaa mbadala kitakachotumika kama paa katika mikoa kumi nayofuatwa. Vifaa hivi vitanunuliwa pia na serikali na kusambazwa kwa namna ambayo wote waliopo katika cheni ya uzalishaji, usafirishaji na matumizi yake utakuwa unaeneza pato zuri kwa wale wanaoshiriki katika kazi hii.

Mikoa inayofaa kutengeneza milango, madirisha na samani nayo itakuwa 10 na watakaoshiriki katika kazi hii nao watanufaika na pato la uhakika katika muda wote wa uhai wa programu ya Nyumba kwa Kila Familia.

Programu isiwazuie wakazi wanaopenda kuonesha utundu na ubunifu utakaotoa dizaini au sampuli mbalimbali za majengo au hata wale watakaoweza kujenga vyumba zaidi ya viwili kwa kutumia akili au ujanja zaidi. Kubwa hapa ni kwamba, ujenzi wa nyumba unapewa kipaumbele cha kwanza na kuwa akili, masikio na macho yetu yote yanaelekezwa huko. Wakati tukijenga matumaini kuwa mwisho wa ujenzi wa nyumba sote tutajipanga vizuri zaidi kutafuta maendeleo na mafanikio ya juu zaidi.

Ujenzi wa nyumba kwa kutumia akili na nguvu za wananchi wetu na msaada kidogo toka serikalini na wafadhili wa ndani na nje. ni jambo linalowezekana. Na hasa ikiwa BOT, Hazina, Kampuni za Simu za Mikononi, Peteroli na Mabenki na Wafadhili wengine wa ndani na nje ya nchi watahamasishwa kuwalipa ujira wa aina fulani wale watakaochangia katika uzalishaji wa vifaa mbalimbali vya ujenzi.

Kwa maneno mengine, endapo kila familia nchini itakuwa na nyumba bora biashara zote zina uwezo wa kukua mara mbili au tatu zaidi kuliko zinavyokuwa kwa hivi sasa.

Programu hii ninaiona ni nzuri kwa sababu fumba na kufumbua ikipata ushirikiano wa serikali inatoa ajira kwa maelfu kama sio mamilioni ya vijana. Kubwa zaidi itajenga imani ya hali ya juu kwa serikali na viongozi wake. Hapa sasa litaonekana angalau jambo moja ambalo serikali imemfanyia kila Mtanzania tofauti na hivi sasa.

Ya kuepuka hapa ni kutokujenga tena nyumba za pamoja karibu karibu sana. Utekelezaji wa mpango huu ni njia pia ya kuondokana na misongamano, foleni na hatari nyingine zinazokuwatishio katika maisha yetu ya kila siku. Nyumba ziwe na nafasi ya angalu nusu ekari kama sio ekari nzima.

Monday, December 20, 2010

Huu ni Wakati wa Nguvu ya Umma

HAKUNA Chama chochote cha kisiasa nchini hivi leo au kesho kinachoweza kudumisha amani, umoja na mshikamano wa Watanzania. Wanaoweza kufanya hivyo ni wananchi kwa umoja wao na katika makundi yao ya kijamii kwenye mtaa, kata, wilaya na mikoa.

Kwa kutambua hili serikali za Tanzania zote baada ya awamu ya kwanza (chini ya chama kimoja) zimegeuka abautani na kukaribisha kwa mikono miwili ujinga, umaskini na maradhi kama njia pekee ya kuhakikisha Chama Tawala kinaendelea kuwa madarakani.

Si kweli kuwa wanasiasa wanaweza wakakubali ujinga uondoke vijijini. Kufanya hivyo ni kuruhusu upinzani kuteka maeneo hayo kama walivyoteka maeneo kadhaa ya mijini.

Rushwa inayotolewa na viongozi vijijini ukichanganya na ujinga na uoga mkubwa wa mabadiliko katika maeneo hayo kunawafanya wanavijiji kile kilicho bora katika kubadili maisha yao-yaani, neema na mapinduzi ya kweli yanayoletwa na demokrasia na mfumo wa vyama vingi.

Kwa kutmbua fika ukweli huu, wanasiasa wa vyama tawala barani Afrika wamedhamiria kuona ujinga unaendelea kuwepo barani humu ili wanufaike na faida zinazoletwa na ujinga huo.

Anayekwambia kwamba kuna kiongozi yeyote wa Afrika anayetaka umasikini utoweke Afrika ni mwongo. Hakuna kiongozi hata mmoja Afrika anayetaka umaskini uondoke.

Umaskini ukiondoka kwanza viongozi hao watakosa fedha za misaada zinazowatajirisha. Pili, wananchi wasiokuwa maskini hawawezi wakayumbishwa na hongo ya kanga, vitenge na pilau.
Na tatu, umasikini ndio unaojenga watu kutokujiamini, ufukara ukitoweka Tanzania basi Watanzania wengi watajiamini na hivyo kuwa huru zaidi kuchagua kile wanachokitaka na sio vinginevyo.

Aidha, kwa kuacha kuitumia kodi ya wananchi ili huduma za tiba na afya zitolewe kiubinadamu na bila upendeleo kwa aliye nacho na asiye nacho serikali yetu kwa makusudi imewageuza wananchi kuwa watu wasio na uhakika na kesho yao.

Vilevile, kwa kuwaonesha wazungu na wageni wengine kuwa wao, yaani, viongozi wetu wa serikali, wanaamini kwamba watu wetu madini yetu na rasilimali zetu nyingine hazina thamani kama wao, mitaji na mitambo yao -watu wetu wamedunishwa na kuwekwa katika udhalili wa muda mrefu na pengine mpaka mwisho wa dunia. Katika hali kama hii, ambayo inakwenda pamoja na kugeuza nchi yetu kuwa jalala la kuuziwa bidhaa duni na za ovyo toka kila pembe duniani basi watu wetu ni muhali kujiamini na kujiingiza katika ushindani wowote wa maana katika dunia hii. Isitoshe, kwa kudharau kuitumia lugha yetu yenyewe na kuendelea kutumia lugha ya kigeni bila nchi hii kuwa na siri wala fikra zake za asili na fasili basi uwezekano wa nchi hii kuja kuzinduka chini ya uongozi wa wanasiasa waliopo hivi leo sio kitu cha kuyumkinika.

Umma hauwezi ukawa unapenda hili au lile, lakini wanasiasa au chama fulani likalazimisha vinginevyo. Kinachohatarisha amani na utulivu katika maeneo mengi ya nchi yetu leo ni kwa wanasiasa fulani kutumia nguvu za dola vibaya, kuikwaza demokrasia na wao kuwaamuliwa wananchi na kuwanyima kile wanachokitaka na kuwapa kile wasichokitaka.

Katika mfumo ambao Chama Tawala kinaweza kuchagua hata watu wenye matatizo kuwa maofisa wakuu serikalini, mabalozi, wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya, wakuu wa benki, wakuu wa mashirika mbalimbali ni dhahiri kwa hapa ndani kwamba maendeleo ya kila mkoa na wilaya yatategemea uwezo au kutokuwa na uwezo wa mkuu anayesimamia husika.

Aghalabu wale wasio na uwezo na ambao wameupata ukuu huo kwa bahati nasibu, huwa ni kombakomba wa kubwa katika kujipendekeza kwa viongozi wakuu. Wakati mwingine hudiriki hata kuvunja haki za binadamu ili kuonesha utii na uaminifu wao kwa kiongozi wa nchi na watu kama hao.

Ni lazima wananchi wetu waeleweshwe kwa kituo kwamba viongozi ni watu kama wao. Na kwa sababu ni binadamu viongozi hao wanaweza wakawa wacha Mungu au wauaji; wanaweza wakawa watu wema au watu wabaya; wanaweza wakawa wezi au watu waaminifu; wanaweza wakawa wakweli au waongo; wanaweza wakawa viumbe wenye utu na ubinadamu au kinyume cha hivyo.

Ili nguvu ya umma ianze kufanya kazi ni wajibu na jukumu la kila mmoja wetu aliyefunguka macho na baada ya kutambua nchi hii ilikotoka na inakotakiwa kwenda kukaa mpango wa kuhakikisha kuwa nchi inakwenda kule tunakotaka iende na sio kule viongozi wachache waliopotea na wasio na uzalendo wa kweli na wa dhati wanakotaka kutupeleka.

Bila kujali sisi ni kabila gani, dini gani, hali gani, jinsia gani na kadhalika tuungane kama kitu kimoja kwanza kwa kubainisha dhahiri ni nini visheni ya kule tunakotaka kwenda. Tunataka tufanikishe mambo gani wakati wa uhai wetu. Tusikurupuke kama wenzetu walivyozoea kukurupuka kila siku na kufanya kazi kizimamoto. Majukumu na wajibu tutakobeba lazima utokane na maamuzi na mipango mizuri ambayo imedhamiriwa kuwepo ili kufanikisha azma zetu za kuwa watu na taifa bora. Maamuzi na mipango inayokataa katakata mtu mmoja au kikundi cha watu wachache kujifanyia mambo jinsi apendavyo bila kufuata katiba, miongozo na sheria tutakazojiwekea.

Lazima wananchi waweze kujipanga kama vile wao ni serikali mbadala kando ya serikali iliyopo ili tuweze kuelimika, kupata maarifa na kujua kile tunachotakiwa kukifanya na kukidhibiti kama tutakavyotakiwa kujua viongozi wetu na watumishi wa serikali zetu wanachotakiwa kukitekeleza, kwa gharama gani, rasilimali gani, ubor aupi na kwa wakati gani.

Kuifupisha kazi hii nitaorodhesha maeneo machache tu ambayo 'Nguvu ya Umma' inaweza ikaanza kuonesha umuhimu, utakikano na sababu ya kuwepo kwake na kuonekana sio tu ipo bali inafanya kazi.

Suala la Katiba. Nchi yetu ina Wanasheria, viongozi wa dini, wanasiasa na mabingwa wa fani mbalimbali wanaoweza kuketi pamoja na kututengenezea katiba mpya.

Kinachoonekana sasa hivi ni kuwa chama tawala kimegawanyika kati ya wataka viraka na wataka katiba mpya. Wataka katiba mpya, kwa kutambua kuna maslahi katika kusimamia kuundwa kwa kariba mpya wanataka kuteka nyara madai ya kuwa na katiba mpya. Wanaelewa fika wakikubali kuwepo kwa katiba mpya basi misaada yote ya ndani na nje itadhibitiwa nao. Na juu ya yote watakuwa katika nafasi bora zaidi ya kutengeneza katiba ambayo itakuwa inawapendelea wao na chama chao.

Wataka viraka, wanafanya hivyo ili kulinda maslahi yao, nafasi zao za kazi au maslahi na mustakabali wa familia na watoto wao.

Ni dhahiri wanaopaswa kusimamia mabadiliko ya katiba hawastahili kutoka kwenye kundi lolote kati ya haya. Ni muhimu waunda katiba mpya wakawa ni Watanzania wasiopendelea chama au kundi lolote la watu hapa nchini.

Mikoa huru kiuchumi na kijamii. Ipo habari eti Zanzibar itakuwa mkoa, huko ni kuturudisha nyuma. Kinachostahili kutokea ni kwa kila mkoa kuwa kama Zanzibar. Ila badala ya mkanganyo wa Urais pakawa na waziri mkuu wa mkoa na baraza lake la mawaziri. Mikoa ikiwa na baraza lake la mawaziri sio rahisi kwa wanasiasa uchwara na wasiokwenda shule kuja madarakani kama inavyotokea sasa kwa wanasiasa wa chama fulani nchini.

Eneo moja la nchi eti kuwa na rais na mawaziri wanaopigiwa kura na watu wasiofikia hata laki tatu na nusu, lakini kupata mameya na madiwani halali na safi tu katika mikoa yetu, bila kuzungumzia kuwa na mkuu wa mkoa anayechaguliwa na wakazi wa mkoa husika na baraza lake la mawaziri ni mkanganyiko mkuu wa kimfumo na haki ya kikatiba kwa wananchi kujiamulia mambo yao wenyewe.

Misaada na Wafadhili. Ni muhimu Watanzania wenye fani za menejimenti, uchumi na fedha kutusaidia kujua na kupromoti aina ya ufadhili na misaada itakayotutoa toka kwenye umaskini badala ya kuendelea kukaribisha misaada inayotupa samaki kila siku badala ya kutupa nyavu sisi wenyewe tukavue baharini, mitoni au maziwani.

Umeme. Watanzania tukingoja mpaka serikali iwe na akili ya kutupatia umeme wa uhakika tutajikuta tunachina si baada ya muda mrefu. Lazima mabingwa wa uhandisi na hususan fani ya umeme na uzalishaji nishati wachukue hatua za kwanza kuanza kutukomboa. Nina hakika wakiketi katika simposia watakuja na mambo mengi ikiwa pia njia mbadala za uzalishaji umeme na hivyo kurahisisha nchi nzima kupata umeme kuliko muda uliopangwa na serikali.

Maji na Umwagiliaji Maji. Huko Moshi kijiji cha KIkavu Chini hakina maji kwa miaka miwili sasa. Wananchi wake maisha na uhai wao ulitegemea kilimo cha umwagiliaji. Hata hivyo, hivi leo hawana maji na ghafla wamejikuta ni watu fukara. Makundi ya kijamii ni muhimu kuzuia jambo kama hili lisitokee. Wakuu wa serikali wanaolipwa mshahara kila mwezi hawana uchungu na hili, na wanasiasa wanaongojea tena kuchaguliwa baada ya miaka mitano hawana habari kabisa.

Maji ni tatizo kubwa zaidi ya vile viongozi wetu wanavyodhania. Haiwezekani wao wenyewe kuwa na majibu ya kutosha katika hili. Ipo haja ya kuongeza kasi ya uanzishwaji wa miradi ya kijamii ili kutunusuru na ukosefu mkubwa wa maji katika sehemu mbalimbali za nchi katika miaka inayokuja.

Shule na Vyuo Binafsi. Hivi sasa kila mtu anajua fika kwamba shule na vyuo binafsi vinatuibia Watanzania kushoto na kulia. Chukulia mfano wa ada ya kati ya milioni 1.5 hadi 2.5 inayolipwa kwa baadhi ya shule ya msingi na kisha mtoto kila muhula kwa mihula mitatu anatakwa awasilishe bunda la karatasi (rim of paper) ambalo moja hugharimu zaidi ya shilingi 10,000. Kwa maneno mengine, ikiwa shule ina watoto elfu moja mwenye shule na walimu wake fumba na kufumbua wanapata shilingi milioni 10 za bure. Hili linafanywa na shule ndogo kwa kubwa ikiwemo zile za watukufu wabunge wetu.

Kama ilivyo kawaida ya wanasiasa wetu na serikali yao-pamoja na kusikia kilio hiki cha wazazi, kwa kuwa baadhi ya wamiliki wa shule hizo wanakisaidia chama tawala, uamuzi juu ya kuundwa kwa chombo cha kuratibu ada na gharama nyingine za shule hauwezi kufanyika haraka.

Uchimbaji Madini. Wapo wenye mawazo kwamba Tanzania iwatumie wataalamu wake wa madini waliosomeshwa ndani na nje, ili mradi walipwe kama wazungu wanavyowalipa wanaowaajiri kutoka kwao na ndani ya nchi, washawishike kufanya kazi kama waliopandwa na pepo. Tukope, tuwe na mitambo yetu wenyewe lakini madini tuyachimbe sisi wenyewe na sio vinginevyo.

Hili halihitaji mchango wa serikali. Matajiri na taasisi za Kijamii zikijipanga uzuri na kwa kushirikiana na wachimbaji toka China, Malaysia, Korea, Uarabuni ambao sio waroho kama hawa waliopo tunaweza kabisa kuhakikisha utajiri wetu wa asili unakuwa utajiri unaowafaa wananchi wetu wenyewe hapa nyumbani badala ya kwenda kuwanufaisha wageni huko nje.

Ajira kwa Vijana. Vijana wengi wa Kitanzania hawana ajira. Je, tukae na kuisubiri serikali ije na miujiza? Au kuna wenye uchungu na nchi hii wanaoweza kuanzisha vuguvugu la kijamii likahakikisha kuwa hili linafanyika.

Nimewahi kuzungumzia juu ya uwezekano wa nyumba kwa kila familia Tanzania. Hebu tuliangalie kwa undani zaidi hapa. Ninachosema mimi hapa ni kuwa ujenzi huo wa nyumba kwa kila familia ni programu ya kipato ambayo inaweza kufadhiliwa na wananchi na wale wanaotakia wananchi wa Tanzania mema na sio lazima serikali.

Kinachotakiwa kufanyika ni kupata fedha ya mbegu ili kuwawezesha vijana wa mkoa au mikoa fulani kuzalisha matofali yote yanayohitajika; kisha wale wa mikoa mingine kupewa jukumu la kutengeneza vigae au vifaa vinavyofaa kuezekea; na kisha wengine wakapewa kazi ya kutengeneza milango na madirisha na vifaa vya ndani. Kwa namna hii, vijana wa kila mkoa watalipwa kwa kazi yao na kisha wanachozalisha kitakwenda kutumika katika ujenzi wa nyumba katika kila mkoa na baada ya miaka 10 mradi huu utakuwa umewanufaisha watu na kuingiza biashara na ajira mpya badala na hivyo kututoa kwenye ngazi moja ya maendeleo na kutupeleka kwenye ngazi ya juu zaidi.

Ni wazi mpango huu ukifanikiwa, nchi nyingi za Kiafrika zitahitaji watu wetu kwenda kwao kuigilizia jambo hili. Neema iliyoje? Swali ni Je, wanasiasa wanaliona hili ?

Nimetoa mifano michache. Hoja yangu i wazi. Watanzania tukidhamiria tunaweza kuondosha umasikini kabisa na kufanya chochote tunachokitaka. Lakini lazima tuepukane kwanza na wajanja ambao wanadhani wanaweza kuendelea kuiibia nchi, BOT, Hazina na wizara zetu mwaka nenda mwaka rudi na nchi ikanusurika na uovu wao. Lazima serkali iwe ya chama ambacho wizi na rushwa kwake ni haramu ndio tu tutaanza kuelekea kwenye njia ya kweli ya kuupiga vita umasikini na kukosa maendeleo.

Ni vigumu kuwazia maendeleo chini ya utawala wenye chuki, uonevu, dharau, dhuluma, wizi, upendaji ukubwa na makubwa bila kuyatolea jasho na wanasiasa wanaoiingiza nchi katika madeni makubwa makubwa na ya ajabu kila mwaka -ambayo yote ni wiiiiiiziiiii mtuuuupu!!!

Watanzania lazima wajipange na kusema waziwazi: 'Hakipendwi chama hapa bwana, tunataka maendeleo. Ubaguzi wa kichama lazima ufe. Na viongozi wawe ni watu walochaguliwa, wanaofaa na wanaoweza kuifanya kazi mbele yao na sio eti tu kwa sababu ni wanachama wa chama fulani. Mathalni, mikoa ya Arusha, Mara na Kigoma kwa hali yoyote ile ilistahili kuwa na uongozi wa Vyama vya upinzani. Pengine hata mkuu wa mkoa na wakuu wa wilaya wakitoka upinzani.' Haya yanawezekana kwa kukataa mifumo iliyopo kupitia katiba mpya itakayoondoa mapungufu yote yaliyoko katika katiba ya sasa.


Contributions to People who Matter!